Sunday, November 18, 2012
Fukara wa uongozi
Ni mkubwa masikini, akosaye uongozi,
Huishia taabani, asipate usingizi,
Raha awe haioni, nyumbani na matembezi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Ukiipanga thamani, kwanza upe uongozi,
Huu ukiwa makini, zote utapanda ngazi,
Dhaifu ukiauni, mazingira huyawezi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Huchahia akilini, pasiwe na mageuzi,
Wenyewe ukajihini, kwa kuukosa uwazi,
Chenga ukaziamini, magoli ni upandizi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Huathirika moyoni, hauwezi maamuzi,
Uliokuwa laini, kwa hariri vitambazi,
Na msingi huuini, kuja kufanza majenzi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Mipango hujizaini, ikawa na utatizi,
Mikakati kutahini, ikawa ni kubwa kazi,
Rasilimali kuhini, ni ajizi si ujuzi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Inapokufa imani, hukuambaa mwenyezi,
Akakuacha uwani, barazani kubarizi,
Ulicho nacho kichwani, tena kisiwe azizi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Atakaye jiamini, aloweza haliwezi,
Ajitiaye imani, anajua uongozi,
Hufulia hadharani, mafichoni ajienzi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Niepushie Manani, mimi kwako si mjuzi,
Pasina yako ilani, kazi hii siiwezi,
Niongoze mashakani, kivulini nibarizi,
Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment