Thursday, November 8, 2012
ITAWAKUSANYA
Kuikunja haijawa, mfukoni kuitia,
Mida imeamuliwa, saa zinajipaua,
Mkono waandaliwa, wa Mungu uliokuwa,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Yaja yasotarajiwa, watu wasioyajua,
Milango ikafungua, darini iliyokuwa,
Pepo wakaachiliwa, duniani kutembea,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Udi wanafukuzia, na harufu twasikia,
Machoni wasiokuwa, dua wanatuombea,
Malaika washangaa, viumbe kuwaigizia,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Innahu yakidunaa, wa akidu kaidaa,
Wote wanaitikia, na ndivyo itavyokuwa,
Hakuna linalokuwa, ila Mola kuridhia,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Yajikusanya dunia, nyaraze kujikusanyia,
Mahemani zikatiwa, au pepo kuchukua,
Yake yalipoanzia, ndiko kule kusokuwa,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Kitu wala haikuwa, na jambo likazaliwa,
Neno lilipotimia, njia iliandaliwa,
Wengi wetu kupotea, wachache njia kujua,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Yenu siwezi yajua, hali yangu sijajua,
Ila ninazingatia, niliyoishaamriwa,
Kisha nikayaambaa, yote nisiyoruhusiwa,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Dunia naihofia, karibu kukaribia,
Mbali mimi nimekaa, siku yangu kungojea,
Na juu nikiingia, pembeni kujikalia,
Hamtokusanya dunia, ila itawakusanya !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment