UA unapochanua, wengi wanakuzengea,
Kila mtu na yake nia, na wewe hautoijua,
Mashairi hukwimbia, marashi yaliyotiwa,
Ua waringia nini, huchumwa kutiwa ndani ?
Hukupamba kwa ridhaa, ukawaka kama taa,
Huchumwa kwenye sinia, birikani kwenda tiwa,
Maji wakakumwagia, ubatizo ukapewa,
Ua waringia nini, kunesa hufika mwisho ?
Bustanini ukiwa, wanesa kwa kutulia,
Upepo kuuringia, na kuihofu mvua,
Uzuri ukaringia, usije kukupotea,
Ua waringia nini, kunesa hufika mwisho ?
Nyuki huwashangaa, kwa wingi kukuvamia,
Utamu ulojaliwa, wakawa waudokoa,
Wakenda jitengezea, kitamu usichojua,
Ua waringia nini, kumbe huwa wanyauka ?
Washtiri hukutwaa, wakenda kujiuzia,
Watu wakakunua, zawadi upate kuwa,
Kisha kuwapelekea, wazuri na wasokuwa,
Ua waringia nini, kumbe huwa wachakaa ?
Kisha kuwapelekea, wazuri na wasokuwa,
Wagonjwa na walofiwa, wote kupata hidaya,
Kumbukumbu kurejea, kumbe nao wahesabiwa,
Ua waringia nini, kumbe hupoteza rangi ?
Harufu hukusambaa, jasmini kawa wawa,
Na waridi la ulua, chuoni ulozaliwa,
Watu wakakusikia, hata kwa mbali ukiwa,
Ua waringia nini, kumbe huwa wachakaa ?
Waume hukutezea, kama picha vile kuwa,
Mashindano kuwatia, wala haya kutojua,
Muumbwa kwenda sifiwa, huwa kweli ajiumbua,
Ua waringia nini, kumbe huwa wachakaa ?
Sifa anayetakiwa, Muumba aliyekuwa,
Yako kukuzidishia, na salama kuipewa,
Usije kuadhiriwa, ikakucheka dunia,
Ua waringia nini, kumbe huwa wachakaa ?
Ila ninachoshangaa, shukurani kutotoa,
Hudhani umezaliwa, wala kuumbwa hukuwa,
Moto ukapalilia, kasri milelel kukaa,
Ua waringia nini, kumbe harufu hukoma ?
Ujana ukipangua, na maungo kupungua,
Tetracycline ukawa, na makengeza ukawa,
Washikaji hukimbia, wengine kwenda epua,
Ua waringia nini, kumbe huwa wazeeka ?
Mvuto ukipotea, nyuki wanakukimbia,
Huhamia palo poa, hai wakajisikia,
Jinai kwao ikawa, wewe kukutembelea,
Ua waringia nini, nyuki huwa wakususa ?
Ujana wala si saa, muda hautotimia,
Kwa wepesi hukimbia, kama radi ilokuwa,
Kufumba na kufumbua, uzee umeingia,
Ua waringia nini, kumbe mvuto huisha ?
Uzuri ukafifia, na mwisho ukapotea,
Kioo ukakimbia, na maji kukupembua,
Ikawa huna staha, ila raha na karaha,
Ua waringia nini, kumbe huwa wakauka ?
Laiti ungejijua, ua utajiangalia,
Muda ukautumia, ya kwako kujijengea,
Na mazuri kuyazua, kizazi kuja kufaa,
Ua waringia nini, hubakia historia ?
<<
No comments:
Post a Comment