Thursday, November 8, 2012
Kila mnachoamua
WENGI ninavyowajua, watasema upuuzi,
Rai wakaikataa, na kuniona mshenzi,
Mimi ninalojua, dhikiri tayari mtenzi,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Siku ikijawadia, nina la kujitetea,
Langu niliwaambia, hamkuwa wa kusikia,
Changu chema 'meachiwa, sintouona udhia,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Mtu hakuninunua, wala sijawanunua,
Sikutumia rupia, ukubwa kuugombea,
Na ngazi sikutumiwa, waovu kujipandia,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Haramu sikutumia, miye nilikikataa,
Wala siri haikuwa, na nyie niliwaambia,
Ila kwa kuipenda dunia, mlitanguliza tamaa,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Kizazi hamkuwazia, utumwani kitakuwa,
Kwa uchu mlichukua, visenti kuvitumia,
Nchi mkajiuzia, bila ya kujitambua,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Wa umoja wakuua, rafiki mkachagua,
Mwalimu alokataa, nyie mkakiridhia,
Gunzi sikio kutia, Nyerere kutomsikia,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Mbali hamkuangalia, mkaiangukia pua,
Njaa iliyowasumbua, amani kushambulia,
Na utulivu kuvia, nchi ikaumbuliwa,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Yafaa kujipimia, wapi pa kusimamia,
Waliotutangulia, daima huwa wajua,
Lipi la kulichagua, na lipi la kukataa,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Mzaha mkifanyia, mtakuja lijutia,
Majuto baba hajawa, sikuzote mwana huwa,
Na ndivyo itavyokuwa, siku itapowadia,
Kila unaloamua, ni thawabu au dhambi !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment