Sunday, November 18, 2012

ASIYETAKA K UKOSOLEWA



Nimeioina tabia, makosa wayakimbia,

Rushwa waliochukua, wakataa kuambiwa,

Kazi yao kuzomea, tumbo wakashtakia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Hii ndiyo Tanzania, inakotawalal njaa,

Tumbo linanunuliwa, na akili kuzitoa,

Moyo wakautumia, haramu kuvichagua,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Kilio anayelia, kiungo ameungiwa,

Sura ukiangalia, watu utawadhania,

Nyuma ukichungulia, mkia unatokea,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Watu changa wawatia, machoni limeingia,

Hao hao walokuwa, tofauti wajitia,

Kuna wanalokusudia, na Mola analijua,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Akili mkifungua, siri mtaigundua,

Si wengine walokuwa, haohao mwawajua,

Roho wamezifulia, kulemaza Tanzania,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Nayo mkiyaachia, vijana kuangamia,

Zuri hamtoambua, balaa inawajia,

Hakika mkichelewa, ng'ombe wayo mwawauziwa,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Ng'ombe wayo mwauziwa, katu nchi haitakuwa,

Miti ikendazolewa, mkaa ukabakia,

Vito mkahujumiwa, na mashimo kubakia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Kitu hamtajaliwa, bali dhiki na udhia,

Heri itawakimbia, shari kuwaingilia,

Akili msipotumia, wenyewe mtaumia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Wachunguzi wanambia, mzungu wanaujua,

Nyumba imeshachafuliwa, na mto unatakiwa,

Maji yake kuingia, makazi safi yakawa,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Kazi kubwa itakuwa, mwaweza kuikimbia,

Ila isipozingatiwa, makubwa yatatokea,

Mkisimama radhia, dosari mtafagia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



No comments: