Sunday, November 18, 2012
NAULIZA TANZANIA ?
Swali najiandikia, na sitaki kujibiwa,
Niacheni kuzubaa, na kisha nikapumbaa,
Ni ligumu ninajua, sio mnavyofikiria,
Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?
Wenyewe wameridhia, na makofi kupigiwa,
Kuuza na kunnua, ni halali imekuwa,
Nini unatarajia, kwa tunakoelekea ?
Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?
Bidhaa tumeshakua, nani wa kulikataa,
Wakubwa wameamua, biashara kuingia,
Wao wajifagilia, wengine ubaya kuwa,
Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?
Rushwa imetunukiwa, nani wa kuikimbia,
Chama kimenakshiwa, rangi zake kuzivaa,
Ukitaka kung'amua, tafsiri kuijua,
Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?
Wahaka umenijaa, anzali nimeshakuwa,
Kila nikifikiria, nashindwa kujitambua,
Watu niliowadhania, wamegeuzwa bidhaa ?
Itajengwa nchi hii, na wanaonunuliwa ?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment