Wednesday, November 14, 2012

Karibu naingojea


Mwendo wangu kutulia, kitu kutokimbilia,

Adhama nawangojea, hodi kuja nigongea,

Ushauri kuombea, na mimi kwenda wafaa,

Karibu naingojea, tutete yenye kufaa!



Mengi nimejionea, na mengi najisomea,

Kila nikiangalia, makosa najionea,

Nani wa kumuambia, na kila mtu ajua ?

Karibu naingojea, tutete yenye kufaa!



Upweke nimenunua, furaha najionea,

Nje nikijikalia, na kuangalia dunia,

Watu wakikimbilia, huko nisikokujua,

Karibu naingojea, tutete yenye kufaa!



Hatimaye husinzia, pepo nikaiwazia,

Umiliki usokuwa, hata wake pia kuwa,

Kitu ukakitumia, kisha ukakiachia,

Karibu naingojea, tutete yenye kufaa!



Hewani huogelea, kwenye mbingu nikakaa,

Jua likanisugua, na nyota kunichekea,

Zikaja nyingi dunia, mimi kuniangalia,

Karibu naingojea, tutete yenye kufaa!



Karibu sijasikia, hapo nilipokalia,

Uzee kumbe si dawa, vijana waniambia,

Nabakia kushangaa, hivi kweli yanakuwa ?

Karibu naingojea, tutete yenye kufaa!



Ila ninaloelewa, umoja sijaachia,

Vingine haitakuwa, hadi mwisho wa dunia,

Ahadi akiridhia, liwalo budi litakuwa,

Karibu naingojea, tutete yenye kufaa!

No comments: