Sunday, November 18, 2012
Usultani wautaka
Hamnao visiwani, sasa bara wabakia,
Kama vile ni utani, vyamani wajipandia,
Ingawa siliamini, ndilo linalotokea,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Umeisha visiwani, bara ndio waingia,
Wanaupanda maweni, na mafuta kumwagia,
Kila nikitathmini, ninashindwa kuelewa,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Huu ni uafkani, kitu gani inakuwa,
Kina nani majinuni, hali wasiyoijua,
Watumia dira gani, huku wanakoelekea ?
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Seyyid Said ngamani, omoni kesharejea,
Kafufukia Omani, mjini akaingia,
Ila sio visiwani, Mrima ametulia,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Na wameanza kuhani, mzimu kuillilia,
Nywele zao kichwani, kalkiti wanatia,
Zipate kuwa laini, umanga kukurubia,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Weusi wauzaini, weupe kukimbilia,
Wajipaka vihinani, ngozi wakajichibua,
Weupe wapate winii, heshima juu kupaa,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Ya wengine si amini, huwa yansiginiwa,
Roho haziwi laini, kwao wasichokizaa,
Ila hutia imani, kwa sadaka kutoa,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Huibia masikini, wenye shibe wakapewa,
Wajumbe wakaamini, nchi watawagawia,
Wasiache usukani, daima kushikilia,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Wajivukiza ubani, na marashi kujitia,
Wakageuza peponi, hii ya kwao dunia,
Wanajua hawaioni, ya kweli iliyokuwa,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Walalao amesheni, sultani kumpokea,
Katokea ugenini, nyumbani anaingia,
Ameona kitu gani, bado mimi sijajua,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
NgazI zao waamini, imara zilizokuwa,
Waanzia vijijini, na mjini wakatua,
Na kisha wilayani, kufikia wa mkoa,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Kisha huja taifani, makungi kujigawia,
Kuuenzi Usultani, kwenye mpya Tanzania,
Wanatafuta waghani, sasa waje wasifia,
Usultani wautaka, waliokuwa hawana !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment