Sunday, November 18, 2012

MPITO


Ndivyo ilivyo dunia, wakati unafikia,

kwa nchi kujapitia, nafasi ya kujizaa,

Kamampya ikawa, au mbovu kuchakaa,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Tumeacha ujamaa, ubepari twakumbatia,

Na mpito inakuwa, vya watu kuvichukua,

Kwa halali ya kuzua, na haramu ya kulea,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Kiwewe wameingia, watu sasa kusifiwa,

Kwa ukubwa kuzidia, na fahari kuenea,

Kila mpenda dunia, yakini ni yake njia,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Waililia dunia, udugu wakidhania,

Na milele watakaa, hawawezi kuugua,

Ila yawanyanyapaa, na wao hawajajua,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Haiwapendi dunia, yawaona ni udhia,

Na hasa mnaokua, watukufu mmekua,

Kila siku inalia, lini mtaondolewa ?

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Yataka badilishiwa, wa heri ikapatiwa,

Si laana kuchukua, kitu isiyosaidia,

Muumba wamuambia, ni nini watufanyia ?

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Dhaifu twahitajia, dhalili waliokuwa,

Wanaokusujudia, na sifazo kuzitoa,

Hadi machozi kulia, kila wakikukumbukia ?

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Mizigo watuachia, kitu isiyotufaa,

Rabana twakulilia, hima kutupunguzia,

Mpito ukiishia, tuje wema kujaliwa,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !





No comments: