Wednesday, November 14, 2012
Tatu ya hatitriki
Swali nimelisikia, shabiki waulizia,
Magoli ya kuingia, hayo vipi yatakuwa,
Matatu yalobakia, nani atajifungia,
Tatu ya hatitriki, msafi au fisadi ?
Ni kando wanaokaa, majeshi wakatumia,
Mipira wakaachia, miguuni kupitia,
Na jasho wasiotoa, ila majibu kungojea?
Tatu ya hatitriki, msafi au fisadi ?
Ni pumzi wa kutoa, au fedha kugawia,
Hongo wakaichukua, magoli kuyaachia,
Tena bila ya kujua, zaidi wangepatiwa ?
Tatu ya hatitriki, msafi au fisadi ?
Au wema walokuwa, sasa tusiowajua,
Mazuri wanayolilia, nchi kuja ambulia,
Na nguvu wasotumia, na hila zenye balaa,
Tatu ya hatitriki, msafi au fisadi ?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment