Sunday, November 18, 2012
MIUNGU WATU
WALE na waitumie, waliokwishajaliwa,
Katu wasinihurumie, wala kuja nigawia,
Razaki nimjuae, yangu atanipatia,
Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !
Ya kwao niwaachia, yangu nitajifanyia,
Pamwe na maruerue, wala siwezi sinzia,
Sintokihofu kiwewe, cha njaa na kuishiwa,
Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !
Naomba nihurumiwe, yangu nikijifanyia,
Riziki nijipatie, ya halali ilokuwa,
Kivulini nijile, hata ni kavu ikiwa,
Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !
Bure usijisumbue, vinono kuniletea,
Nenda navyo katumie, wewe kukusaidia,
Kiporo changu nachie, kukila naendelea,
Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !
Mola wangu sio wewe, wala hauwezi kuwa,
Hili bora uelewe, vingine kutodhania,
Na moyo uufunguwe, ujue unaugua,
Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment