Sunday, November 18, 2012
Leo mnaowaabudu
KAENI mkitambua, ukweli utabakia,
Nasi tuliwaambia, hamkutaka sikia,
Miungu mnaozaa, watakuja waumbua,
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Sauti naisikia, ya saba inatokea,
Kukana mlilozua, kuwa yeye amezaa,
Uchuro aukataa, na wala hakuzaliwa,
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Warumi wawahadaa, yak wao kuyafatia,
Miungu wengi tabia, ndio wao walozua,
Wapenda kuwashindilia, kikapuni wakakaa,
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Kunaye wao wa mvua. na kisha kuna wa jua,
Huba naye kajaliwa, ana wake kawekewa,
Na wa mavuno hupewa, sadaka akaachiwa,
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Mola asikitikia, wasomi wasiosomea,
Hata kitu kukijua, na yakini kuitia,
Kama wana mnakuwa, uzushi ukawafaa ?
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Mola awahurumia, vitabu msiojua,
Moja mkajishikia, hakika lisilokuwa,
Kama vipofu kupewa, nafasi tembo kumjua,
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Yupo aliyeringia, tembo ni kama sinia,
Na mwingine kaingia, ujuzi ajivunia,
Kama shina anakuwa, tembo ninayemjua,
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Wote walijipatia, sehmu waliyoachiwa,
Zaidi hawakujua, kwingine kuyagundua,
Na Alamu muelewa, ndivyo anatufanzia,
Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment