Sunday, November 18, 2012
Mshairi sikuhizi
Waliozoea hadhi, kwa ubwabwa na mandazi,
Washairi sikuhizi, huwa haviwapendezi,
Waelimika wajuzi, kuyatafuta azizi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Wanaotafuta mapenzi, wale sifa za Muizzi,
Kitu hawaokotezi, wakataa ubazazi,
Hali mashehe wa enzi, wafulia kwa hirizi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Ajijua si mkazi, majoho hayadarizi,
Wala siye muamuzi, ya watu hayatatizi,
Ajijua kiongozi, njia bora msimamizi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Huyu ni muangalizi, kuukataa ushenzi,
Tukamhofu Mwenyezi, na dunia kutoenzi,
Wala hanayo ajizi, yakitua mageuzi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Hakika ni muenezi, ya ovyo hayatangazi,
Asiyekwaza uwazi, iwe jana au juzi,
Ya umma ni mdowezi, haumalizi utenzi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Mipango ni msimamizi, mizuri si ya kichizi,
Kuyaleta mapinduzi, vya msingi kuvienezi,
Maji yakawa utenzi,usioisha simulizi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Chakula kikawa dozi, hakikosi mwanagenzi,
Vijiji wakapalizi, na mjini kuhifadhi,
Pakafanzwa na makuzi, uuzaji na uzuzi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Nyumba zataka ujenzi, kama la kwanza zoezi,
Watu ukiwahifadhi, mengine watafaridhi,
Pakiwa nayo ajizi, ufukara uko wazi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Hapanao utetezi, ila siasa chukizi,
Zitakazo kujienzi, na wengine kuwaizi,
Kwangu mimi machukizi, walal hazina hifadhi,
Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,
Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment