Wednesday, November 14, 2012
Kuringa kukigeuka
Mringaji 'kiringiwa, vipi anajisikia,
Mkausha kukaushiwa, macho vipi yanakuwa,
Na mnuna akununiwa, roho huwa yamtua ?
Kuringa kukigeuka, ikawa ni kuringiwa !
Haya ninaelezewa, bado ya kujionea,
Kama picha imekua, hisia zasisimua,
Ila yakinitokea, ukweli nitaujua,
Kuringa kukigeuka, ikawa ni kuringiwa !
Ukisha kuzuzuliwa, hukubali kuringiwa,
Kukiisha kuringiwa, hubakia na mafua,
Maana kilichokuwa, udhia kikabakia,
Kuringa kukigeuka, ikawa ni kuringiwa !
Mapamba yakikuhadaa, kehso yake hujijua,
Sio kitu ulokuwa, bado una yako njaa,
Jana uliyekimjua, leo hatokutambua,
Kuringa kukigeuka, ikawa ni kuringiwa !
Ndivyo ilivyo dunia, kuringa na kuringiwa,
Kila anayetumiwa, hataukwepa udhia,
Mifuko ikikujaa, mzuri huchukuliwa,
Kuringa kukigeuka, ikawa ni kuringiwa !
Mzuri huchukuliwa, mifuko inapokujaa,
Ila unaposhiwa, ubaya hutafutiwa,
Na mwisho ukazuliwa, hata chako kutwaliwa,
Kuringa kukigeuka, ikawa ni kuringiwa !
Dunia nguli wajaa, kazi yao ni ubaya,
Wanyonge huwaonea, na wale wasiojaliwa,
Thamani wakatolewa, na hasidi kupakiwa,
Kuringa kukigeuka, ikawa ni kuringiwa !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment