Sunday, November 18, 2012
JAMBAWAZI WA UKWELI
Huyo huwa ni kibaka, jambawazi hatokuwa,
Mchana anayecharuka, jirani kuwaibia,
Uteja unampika, hamu budi kuridhia,
Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !
Haibii masikini, jambawazi wa ukweli,
Huona ni uhaini, mkubwa uso mithali,
Wenzie hawamwamini, budi kumshtakia,
Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !
Awajua masikini, vipi atawaibia,
Awanyime afueni, mautini kuwatia,
Kafiri na muumini, huiona ni hatia,
Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !
Ukiwaona mjini, fukara wawaibia,
Uwajue kwa yakini, ni mateja walokuwa,
Kamwe hawana thamani, masikini kuibia,
Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !
Wakatia mafichoni, Uswizi kwenda chimbia,
Huku njaa taabuni, kila mtu analia,
Ya kwao madhumuni, hakika ni kutuua,
Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !
Wanatuona ni nyani, thamani wanatutoa,
Na vyao waamini, ndivyo vilivyojaliwa,
Hakika ni hayawani, wenda uchi pasi 'jua?
Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !
Wa ukweli ajijua, kwa watu ataka nini,
Si kununua udhia, au wengine kuwahini,
Maisha ayaelewa, na uhai athamini,
Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment