Sunday, November 18, 2012
Tusingoje ya U.S.S.R.
U.S.S.R. jua, ilishaaga dunia,
Jambo hili latwambia, kitu tusichotambua,
Vigumu kufikiria, na gumu kuaminia,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Ni vipande imekua, hadithi twazisikia,
Waloleta ujamaa, walipojipendelea,
Ukweli ulipotua, wakaonwa ni wabaya,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Sasa stani zajaa,na kina Bylorussia,
Wapo kina Georgia, watu kunakozingua,
Pia nayo Chechnyia, watu wanayohofia,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Palikuwa na Rhodesia, hivi leo twasikia,
Zimbabwe na Zambia, ndizo hizo zilikuwa,
Kumbe nchi hujifia, kiyamache kikingia ?
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Ndivyo ilivyo dunia, yake inavyomboa,
Na asiyejitambua, hutaka kung'ang'ania,
Shauri asiposikia, haachi kujiumbua,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Si mbaya ujamaa, bali watu wa dunia,
Ujanja wakiutmia, matope hukupakaa,
Kizuri kilichokuwa, kuonekana kibaya,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Nchi zinakufa pia, ukitawala udhia,
Ngapi umezisikia, zimeiacha dunia,
Kumbuka Babylonia, zama ikihadithiwa,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Kunayo Mesopotamia, ilitawala dunia,
Uyunani nayo pia, wote tulishaelezewa,
Makuu waliyazua, mashine pasi gundua,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Misri twahadithia, ya zama ilivyokuwa,
Leo taka imekua, watu waona kinyaa,
Farao hajatokea, nchi kuja inyanyua,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Palikuwa na Persia, michezo twaisikia,
Mabinti waliong'aa, hadi wakapiganiwa,
Watu roho wakatoa, ili kwenda zawadiwa,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Palikuwa na himaya, Afrika twazijua,
Wachamungu kuwazua, kama Mali nasikia,
Hivi leo nayojua, si kitu ila balaa,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Marikani kulikuwa, na kubwa pia himaya,
Wahindi wakupakawa, huko walizinyanyua,
Dhahabu wakatumia, nyumba zao kujengea,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Tanganyika tuliua, mochwari hatukutoa,
Nimekwenda angalia, naona inapumua,
Na sauti kusikia, 'nawe utanipigania? '
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Naam, nikaitikia, bila ya kujitambua,
Labda nilihofia, maiti kuangalia,
Au baridi kukoa, kitu sikukitambua,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Kungi wanihadithia, mapenzi yanavyokuwa,
Mwana ukishamridhia, kambaye ni kumuachia,
Hunenda akatembea, au mbali kwenda kaa,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Ila kwawe kumuachia, huru atajisikia,
Ngamani atarejea, hema akalichimbia,
Na penzi juu likawa, hatolishusha radhia,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Kama ukimshikilia, na wivu tele kujaa,
Huyo atakukimbia, na wala hatarejea,
Ndivyo ilivyo dunia, mamboye ni kuyaachia,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Hili nilipogundua, mwepesi wa kuatia,
Usumaku nakataa, sitaki kung'ang'aniwa,
Biriani napindua, na kisha kuuachia,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Rangize kujitanua, chembe mojamoja kuwa,
Siniani kitulia, siriye hutoijua,
Sikio ukifungua, hunong'onezwa na jua,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Mrima na Zanzibar, nadhani mwanisikia,
Uziwi sijaujua, hiyo nyingine balaa,
Naomba kutojaliwa, ili sote kujaliwa,
Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment