Thursday, November 8, 2012

Watumwa wangelikuwa

MBALI sana haijawa, toka karne kuishia,


Utumwani tulikuwa, watu tukinunuliwa,

Leo tena yarudia, yaleyale yalokuwa,

Watumwa wangelikuwa, elfu moja mia nane :

wajiuzao raia !

Kila unaloamua



Watu wanawatumia, fedha kuwamiminia,

Kisha wakazitumia, raia kuwanunua,

Ili kunyanyuliwa, huyo anayewanunua,

Watumwa wangelikuwa, elfu moja mia nane :

wajiuzao raia !



Yeye amejichagua, kati wote Tanzania,

Kuwa mafuta katiwa, na shetani tusomjua,

Mkubwa wetu kujakuwa, kuongoza Tanzania,

Watumwa wangelikuwa, elfu moja mia nane :

wajiuzao raia !



Ngawira ukigawiwa, usiache kupokea,

Mkono utautia, kinywani kuambulia,

Ila imani hofia, motoni kutoingia,

Watumwa wangelikuwa, elfu moja mia nane :

wajiuzao raia !



Ila imani hofia, motoni kutoingia,

Haramu kilichokuwa, huja kikawa mkaa,

Milele ukaungua, kwa visenti vya hadaa,

Watumwa wangelikuwa, elfu moja mia nane :

wajiuzao raia !



Kisha tena fikiria, kizazi kununuliwa,

Utaileta balaa, rushwa kote kusambaa,

Tukawa ni Nigeria, kwa masahibu na balaa,

Watumwa wangelikuwa, elfu moja mia nane :

wajiuzao raia !



Akili umejaliwa, watakiwa kutumia,

Kila anayenunua, naye amenunuliwa,

Hivi ni yake bidhaa, mwenzangu unaijua?

Watumwa wangelikuwa, elfu moja mia nane :

wajiuzao raia !



No comments: