Sunday, November 18, 2012
Yangu hayana maana
Mimi daima mtwana, wala sijawa ni bwana,
Huo nilishaukana, kuritadi sina dhana,
Hunena ya kufanana, viumbe yakalingana,
Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !
Huwaachia mabwana, propaganda kuchuna,
Roho zao za ujana, bado zajaa hiana,
Wamkana maulana, utukufu kuuvuna,
Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !
Kwa yao ninapingana, uongo unaposana,
Kweli wakaitafuna, si ya leo siyo ya jana,
Ikawa yalia jana, kabla kila adhana,
Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !
Ikawalani amana, na kuiteza dhamana,
Yawarudi na wana, pasiwe na uungwana,
Mengine kutabanana, kwa usiku na mchana,
Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment