Thursday, November 8, 2012
Muogopeni Muumba
Muumba muogopeni, msiogope binadamu,
Amewaumba Manani, kwa ibada kumkimu,
Mengi hapa duniani, kwa haki yamdhulumu,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Ya haki yaamueni, apate kuwarehemu,
Mkijifanya afkani, wenyewe mwajidhulumu,
Mtakuwa mashakani, akhera na duniani,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Wanapozuka wahuni, nafsi kuwadhulumu,
Wao mkawathamini, na kuwaona muhimu,
Linamuudhi Bathini, na yake huwa adimu,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Ni mkubwa mtihani, daima unaodumu,
Saburi na shukrani, akosaye hajihimu,
Ya kesho huwa haoni, aona ya uhadimu,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Humpendeza shetani, na wala sio Karimu,
Akajitia thamani, kwa kuwa hajifahamu,
Kumbe yeye majinuni, na wala hajituhumu,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Hujidanganya kundini, akajiona adhimu,
Kumbe si kitu duniani, hawezi kutakadamu,
Asubuhi na jioni, huwa inaisha zamu,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Watakuja akhirini, nao piTa binadamu,
Wakaingia njiani, jukwani kuhudumu,
Kama wale wa zamani, na wote hatutadumu,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Twendako tuogopeni, tulipo twapafahamu,
Huko kwetu ugenini, nani wa kutukirimu,
Miaka ihesabuni, si viumbe wa kudumu,
Muogopeni Muumba, msihofu binadamu !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment