Sunday, November 18, 2012

Chema utakitambua




Hauachi kukijua, wema kilichojaliwa,

Ishara utazijua, ukianza na tabia,

Huziangalia hatua, kila anapotembea,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Mkamilifu radhia, kwa hulka na tabia,

Na moyoni ana hawa, wanyonge kusaidia,

Kujikweza hukataa, chini hutaka bakia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Si wa kujitangazia, wala wa kujisifia,

Utumwa kauridhia, watu kuwatumikia,

Suti atazikimbia, na kanzu kujivalia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Hariri hatochagua, ila pamba hutumia,

Daladala kupakia, gari akalikimbia,

Watu huwaangalia, si mali kukimbilia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Anaijua dunia, kioo cha kutambia,

Kuvunjika yake njia, na vingine haijawa,

Yenyewe yabakia, watu hawatabakia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Huishi akitambua, maisha kutumikia,

Kama watumikiwa, utumwa unaingia,

Mwenyewe atayavaa, na kisha akajivua,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Daima hujichekea, pasina kumtambua,

Tabasamu lake poa, vigumu kujionea,

Na anachokichekea, mwenyewe anakijua,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Dunia aishangaa, upepo kukimbilia,

Akili wanaopewa, wanashindwa jitambua,

Huko huko kuishia, hadi mvi kupaua,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Utani ajionea, jinsi tulivyoumbiwa,

Hakuna cha kubakia, majivu tu yabakia,

Kisha hujiangalia, akacheka na kulia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !





No comments: