Thursday, November 8, 2012

VICHOCHORO NAVIJUA



Bure mwapotea njia, kwa kushindwa ulizia,

Ububu mnajitia, kiburi uliokoa,

Kila mnachotumia, bure ninajipatia,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Katika hii dunia, ya kula na kugawia,

Mwenyewe ukijilia, wengine walale njaa,

Mwisho watakumbia, mwenyewe ukabakia,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Kila mwenye kujijua, kamba refu huachiwa,

Vyema apate potea, asifike kwelekea,

Kinyume kwenda ingia, mbali akapotelea,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Wapo wanaozaliwa, vibaya wakalelewa,

Tabaka wakanunua, juu wawe waelea,

Hata ya kusalimia, kwayo wawe waugua,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Ndipo yanapotukia, ya kushindwa ulizia,

Kujua wakajitia, njia wasiotambua,

Mkenge kwenda ingia, kama si mmamba kuwa,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Ofa ninawagawia, wasiyoitegmeea,

Kubalini kutojua, wapo wa kuwasaidia,

Yote tukayachambua, na njia kuigundua,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Miaka imesalia, michache iliyouwa,

Hadaa kwa teknolojia, hapo mwaja kufulia,

Ndimu zilizokomaa, chachu yake hupungua,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Chachu yake hupungua, kama chungwa kuja kuwa,

Kama ukilikamua, juisi hujipatia,

Hili ninawaambia, mpate kufikiria,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Fikra ukiishiwa, huwa ni ngumu dunia,

Usiwe wajitambua, kuwa uchi umekaa,

Uwe unajidhania, suti bora umevaa,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !



Malezi mwana kulewa, ajizi nyumba ya ukiwa,

Halisimami gunia, tupu lililobakia,

Na hauwaki mshumaa, pasina kujiwashia,

Njooni mwonyeshwe njia, vichochoro navijua !

No comments: