Sunday, November 18, 2012
Tukaishi vijijini
Vijiji twavikimbia, sana mbali vimekaa,
Hakuna kwenda kukaa, sikuzote kutembea,
Kwalo ninalishangaa, vipi vitaendelea ?
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Kila mtu kaamua, mjini kukimbilia,
Serikali na jamaa, yao moja limekuwa,
Sasa watu waingia, na jioni kuambaa ?
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Kila nikiangalia, hduuma nazigundua,
Sana zimeshafulia, na kisha kuchafuliwa,
Hali yadharauoiwa, kukaa wanakataa,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Maji safi nahofia, kwingi yameshapotea,
Bomba zimeshachakaa, ardhini yakimbilia,
Palipo nalo jipya, kuti kavu wakalia,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Umeme wahadithiwa, lini kuja kuingia,
Mahala ukitokea, watu washerekea,
Miaka ingelikuwa, tayari unatolewa ?
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Huduma za kutitia, kwa elimu na afya,
Kiwango chini watoa, mizania yakataa,
Kila ukifikira,kizazi kinaonewa,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Sasa nimeshaamua, kijijini kwelekea,
Na karibu naitoa, kwa wanaofatilia,
Naenda kusaidia, viwango kuvinyanyua,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Pwani naenda anzia, vijiji kuzungumzia,
Hoja nimejipangiwa, udhaifu naujua,
Kama wakinisikia, pamoja kuendelea,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Naitaka jumuiya, ya kwake kuangalia,
Akili kuzitanzua, tuanzapo kupajua,
Na kisha kuvichambua, vifaavyo kujifanzia,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Maji la kwanza likawa, kijijini kuingia,
Kisha nyumba kuandaa, mkakati wa kuzua,
Kufumba na kufumbua, kijiji kipate ng'aa!
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Huduma zikafatia, ili kilimo kukua,
Usafiri kuutia, urahisi kuridhia,
Kisha tukaangalia, wengine kuwavutia,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Utalii kutumia, kipato kuongezea,
Huku ninajisomea, na vitendo kuvizua,
Naikataa nadharia, feli nimeziamua,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Mola ninamlilia, ndoto zangu kuridhia,
Kusoma huku kukawa, kunaleta manufaa,
Jamii ikichanua, na moyo wangu kuchanua,
Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment