Friday, November 2, 2012
Mbegu za demokrasi
Tisini nimeanzia, mbegu hizi kuzigawa,
Mwanzoni kwenye ukiwa, watu hawakuelewa,
Hivi sasa yamekua, na wenyewe wanunua,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Kumbukumbu maridhia, na mimi nilichangia,
Kidogo kilichokuwa, kama tukifanikiwa,
Kulea demokrasia, na dikteta kuzuia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Vyama vingi kuanzia, hadi vilipoingia,
Mbegu nimezitia, kitabu cha Tanzania:
Chama kimoja mwaa, vyama vingi kuwa njwaa,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Katiba tukaingia, watu wabana kimya,
Hadi wakastuliwa, kelele nilipotoa,
Haraka yakaundiwa, yawe na yasiyokuwa,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Hapa kwenu kuchangia, mjitokeze Tanzania,
Mawazo bora kutoa, katibani kuingia,
Fursa kutoachia, la kwako kutojaliwa,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Tume nayo kufatia, katiba halijaishia,
Sababu sijaijua, kwnaini tunachelewa,
Haki inayolaliwa, ni dhuluma inayokua,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Kisha huru mgomeba, haraka kuamuliwa,
Uchumi kusaidia, mafedha wakayawa,
Waliojaa tamaa, hapa hawatachelewa,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Moyo huwasukumia, haraka wakaingia,
Na wakisha kununua, hamna kujivunia,
Ndivyo inavyotakiwa, kustawi demokrasia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Kuwa chini ya sheria, rais pia raia,
Vingine haitofaa, mchezo tutachezewa,
Nani wa kuaminiwa, katika hii dunia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Kipato kukiamua, nani zaidi kupewa,
Daktari kuchagua, au mwalimu kupewa,
Na wabunge kuamua, walipwe kwa tasnia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Wanasiasa balaa, cha juu wakiambua,
Ovyo wanakitumia, hongo kote kuzitoa,
Mno twawazidishia, kufuru wajifanzia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Katiba inatakiwa, sawa kutuwekea,
Watu wakaendelea, si kwa siasa kuingia,
Ila pale walipokuwa, juu waweze fikia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Juu waweze fikia, siasa chini zikawa,
Wachache kukimbilia, kama Norway ilivyokuwa,
Huko ni wenye nia, ya watu tu kufaa,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Elimu nategemea, ya bure kujifanzia,
Madini ya Tanzania, na mafuta yaingia,
Fedha zake kutumiwa, wana kutusomeshea,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Afya na tiba pia, bure budi kutolewa,
Ni huduma ya jamaa, kila mtu hufikia,
Siku akahitajia, asiikose raia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Rushwa mkiikataa, na usafi kulilia,
Mahala itafikia, nchi bora hii kuwa,
Namimi nawaombea, Mola kuwasaidia,
Mbegu za demokrasi, nimegawa kapandeni !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment