Wednesday, November 14, 2012
Wote adawa wakiwa
Wote adawa wakiwa, rafiki awe ni nani ?
Hivi unafikiria, au sasa hayawani ?
Kuua na kuuliwa, iwe ndio yako shani ?
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Unaweza kupagawa, ukaingia kichaa,
Mafuu ukishakuwa, huna utalotambua,
Utaabiri mitaa, makopo kuyaepua,
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Shuruti yakutumia, kama maji ni kupoa,
Kuna njia hufikia, pemeni kujikalia,
Hali ukaichungua, wapi unaelekea,
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Ndipo unapogundua, binadamu ni hadaa,
Machoni kajifichia, na moyoni kuitia,
Akaifua na haya, na aibu kuitoa,
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Hutaka kukutumia, na wala si kumtumia,
Kila akikusadia, lake anafikiria,
Aweza akalichopoa, haraka kujiondoa,
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Mwema nawakubalia, watunzi waliyozua,
Hakika hajazaliwa, ila waovu wajaa,
Hii ni yetu dunia, ndio mambo yake haya,
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Waongo hukuzidia, ndiyo juu wakakaa,
Wewe ukawadhania, ndio wanaokufaa,
Kumbe wanakutumia, wende walikokukusudia,
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Yako ukenda fulia, hilo halitosumbua,
Ya kwanza kuangalia, ndio ahadi watiya,
Vingine haitakuwa, laiti ungelijua ?
Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment