Sunday, November 18, 2012
Mtumwa akishalewa
Mtumwa akishalewa, shairi hujitungia,
Pombe akaisifiwa, na mpishi kupambiwa,
Kisha akawarukia, uhuru wanaolilia,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Kicheko hukiangua, habari akisikia,
Kuna wanaolilia, uhuru kujipatia,
Ya kwao wakaamua, wapate kuendelea,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Senti imemlevyea, hawezi jielewa,
Kichwani imeingia, ya kutunzwa na kupewa,
Uimbaji anajua, bwanawe kumsifia,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Hii ni yenu dunia, mbingu sijaandikia,
Huku yao wnajua, uhuru walishapewa,
Ila nyie wa kuwia, msiowia raia,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Mtumwa anaridhia, bwanawe kumtumia,
Chakula akipatiwa, hanalo la kuamua,
Kutumwa anangojea, kwingine asokujua,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Shurubu huidhania, yeye ameandikiwa,
Ndivyo alivyozaliwa, lingine kutotegemea,
Mnyenyekevu huwa, hata panapo udhia,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Hujikunyata mkiwa, mama akitulkaniwa,
Uso akakumbatia, milizamu kuzuia,
Huwa anafikiria, haki yake inakuwa,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Haki yake inakuwa, yeye akatukaniwa,
Kisha akadhulumiwa, na budi kuitikia,
Vingine akiamua, ni mkosa yeye huwa,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Huituhumu dunia, kuwa inamuonea,
Kumbe yeye karidhia, kile kisichoridhiwa,
Na tokea kuzaliwa, ni huru aliyekuwa,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Dunia ihofia, kuwa itamchezea,
Akashindwa kutambua, akili katunukiwa,
Naza akizitumia, ufukara huua,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Wanaokung'ang'ania, kuna lao waambua,
Fika wanalitambua, hasara kukuachia,
Mwenye njaa wanjua, ni rahisi kutumiwa,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Ndivyo ilivyo dunia, wajinga hufurahia,
Hawajengi huezua, hata waliyojengewa,
Wa kale wangelikuwa, haya wangeliyakataa,
Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment