Wednesday, November 14, 2012

SIKU HII Tanzania

KIU wengi wazidiwa, maji wanayalilia,


Na wanayoyasikia, miradi wakipangia,

Ila hat alile la dawa, maji hayajaingia,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Waishi Watanzania, hata kando ya maziwa,

Nako ni kizaazaa, maji pia yapotea,

Wengine wayachukua, kwenda kwao kuwafaa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Maji wengi twafulia, sio kwa kusafishia,

Ila nayo kutokuwa, na uchafu unajaa,

Sasa dhiki imekua, hata ua kunyweshea,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Chakula chazidi paa, bei twashindwa fikia,

Na hali ukiangalia, ukali waendelea,

Itakuja kufikia, mlo kutoambulia,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Shangwe ninazihofia, zisijekuwa kulia,

Matumbo yakiadhiriwa, hifadhi kutopatiwa,

Vijijini wakavia, zaidi kudhulumiwa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Gizani tunaingia, asubuhi kuamkia,

Na nyimbo tunasikia, tatizo kuliondoa,

Miezi inaishia, hadithi yaendelea,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Mashine wazilipua, katakata kwendelea,

Hakuna wa kufidia, mtenzi azawadiwa,

NI za kichizi sheria, laiti wangezijua,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Kweli wapo wa kung'aa, njia zao wazijua,

Hawa ukijionea, pepo utaidhania,

Ila wengi ninajua, hali leo zawaua

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Siwezi jihurumia, afadhali naijua,

Nyuma sijaangalia, naitafuta afua,

Ninamsihi Jalia, hili kujaniridhia,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Gharama zazidi paa, kwa elimu na afya,

Mikopo yatukimbia, wakubwa kuwafatia,

Kile tunachobakiwa, yabidi kupigania,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Ni huzuni imekuwa, tena mkubwa ukiwa,

Kesho tunaihofia, jinsi itakavyokuwa,

Utabiri nakimbia, mimi siwezi kutoa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Mola ninamuachia, kadari kuiangalia,

Dhiki kutuepushia, toba zetu kisikia,

Nasi tuongeze dua, tupate kuhurumiwa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !





No comments: