Sunday, November 18, 2012

DHAMANA



Ukubwa mkiupewa, wakubwa hamjakuwa,

Vibaya mwachukulia, hicho mnachoachiwa,

Madaraka huachiwa, sio ya kuyachukua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Mwaachiwa kutumiwa, kwa haki inavyokuwa,

Nyenzo hii hutumiwa, walio wengi kufaa,

Ndipo sawa inakuwa, sio vingine kwamua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Wewe ukiiutmia, mwenyewe kutumikiwa,

Ukapata manufaa, halali yasiyokuwa,

Ni wizi watumia, wala sawa haijawa,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Kaziyo kutumikia, na sio ya kutumiwa,

Kama hivyo inakuwa, unaianza balaa,

Vipi kukuchukulia, kiongozi ulokuwa ?

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Yataka kujisimamia, la halali kulijua,

Muumba akakujua, uongozi wakufaa,

Sio ukanyenyekea, kile tusichokijua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Mamlaka ya raia, haki inavyotambua,

Katiba inalijua, waziwazi linakuwa,

Ila huzuka hadaa, watu wakazainiwa,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Wenye vyeo kudhania, nchi yao imekuwa,

Ovyoovyo kuamua, na ya kweu kukataa,

Hilo mwisho lafikia, macho wameshayafungua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Heri hili kutambua, tujenge demokrasia,

Ya kweli iliyokuwa, wala sio ya snaa,

Mida imeshaingia, mageuzi kuingia,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Pepo zinakurubia, nafasi kuichukua,

Ombwe nje kulizoa, la haki kuzingatiwa,

Mwaka hautoishia, mengi tutayasikia,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !





No comments: