Thursday, November 8, 2012

MSAMBE SIKUTETA





Njia nimeipitia, na mwisho sikuishia,

Mimi ni mpita njia, wengine ninaachia,

Niliyokwishapangiwa, yaishia kutimia,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !



Akili nilifungua, ukweli kuangalia,

Niliikuta hadaa, kona zoe imejaa,

Nchi inauogea, na wengine wafulia,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !



Mengine nilidhania, kinyume chake ikawa,

Maji yalinikatalia, kwenye gunia kujaa,

Tope yameniachia, miguu kunichafua,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !



Na kila mnunuliwa, sasa ananichukia,

Kafara kuikataa, mizimu haikutwaa,

Hakuna kilichobakia, uoza umebakia,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !



Yapo yasiyojaliwa, kisirani yanakuwa,

Balaa kutangulia, zahama nayo mabaa,

Wafu huja kuzaliwa, na vichanga kufukiwa,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !



Nuru wenyewe huua, giza wakashangilia,

Linapowaelemea, wakashindwa vumilia,

Wakawa watu wa kulia, kushoto wasiojua,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !



Shetani msipomkimbia, yeye hatowakimbia,

Ukuraba ni furaha, apenda kufurahia,

Ila hukumu ikiwa, nyie atawakimbia,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !



Vipofu nashuhudia, haya walijionea,

Na viziwi kusikia, Tanzania italia,

Ila hawakuyasikia, wale waliotegemewa,

Msambe sikuyateta, mkajitia uziwi !

No comments: