Thursday, November 8, 2012

Kukomoana






Mswahili anajua, kinyozi huwa hajinyoi,

Labda ingelikuwa, kwa mashine yuko hai,

Bali hilo ninajua, kwenda mbele hajawahi,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Hapa tulipofikia, hili siwakubalii,

Kazi yangu kuchochea, kutafuta ustawi,

Vya watu mkitumia, kitu hamuambulii,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Humshangaa mjua, aliyekuwa hajui,

Ujibari kujitia, sumu asiikinai,

Lusifa hajatambua, ni rafiki si adui,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Uerevu kajitia, naye mvaa kikoi,

Na jana hakujijua, wala kuwa nayo rai,

Ila leo kajaliwa, mbwa mwitu alo mwui,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Kaikoleza tabia, hajifai kwa nikahi,

Uraibu aitia, hata inakuwa hoi,

Kisha kujitapikia, ili hali hajijui,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Husuda imemjaa, kitanzi hakiachii,

Mashavu yamemjaa, gubu halimuachii,

Aibua na kuzua, ya watu kutoa uhai,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Alalia, aamkia, na sala kaisabahi,

Huku utu ajitia, na shetani amrai,

Mushiriki amekuwa, Afu hamuangalii,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Tadi na inda zajaa, wala kwake si jinai,

Moyo kutu waizua, ya ndugu hafurahii,

Si wa kujitambua, kafa ili ayu hai,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Akili ameishiwa, hili lile hayajui,

Chombo anakitumia wengine walichokinai,

Na mishipa yamjaa, kwalo hilo kazirai,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



Kaishia muishiwa, kwa Mumiti na Muhyi,

Ameishaingiliwa, alimoko humtoi,

Ila litamuumbua, vuvuzela likirai,

Usinikomoe mimi, ukajikomoa wewe !



No comments: