Sunday, November 18, 2012
Aali wastahili
Akili zikifulia, madoho huyaridhia,
Mbali hautoyajua, wala hutojionea,
Yako ukayadhania, ni makubwa yamekuwa,
Aali wastahili, tumeangusha wananchi !
Yetu ukiangalia, sisi nyuma twabakia,
Sote tulipoanzia, sawasawa ilikuwa,
Kundi ukilichukua, twadorora Tanzania,
Aali wastahili, tumeangusha wananchi !
Ni bure kujisifia, kwa ukweli lisokuwa,
Ili wende hurumiwa, wembe ukiandaliwa,
Kinyozi hajajinyoa, naye huomba nyolewa,
Aali wastahili, tumeangusha wananchi !
Ila walioingia, mashine wanatumia,
Hiyo hiyo hutumia, na wao wakajinyoa,
Kisha wakatuzingua, na hasira kututia,
Aali wastahili, tumeangusha wananchi !
Mengine ni kunyamaa, sauti kutotoa,
Chumvi ukizidishia, chakula hakitaliwa,
Kwanza mngeliyajua, uzito kujipimia,
Aali wastahili, tumeangusha wananchi !
Pande mkaangalia, ni wapi imezidia,
Kama kwenu imekua, hayao yenu manufaa,
Wengine huangalia, kama wana manufaa,
Aali wastahili, tumeangusha wananchi !
Kitu wasipoambua, vipi watakusifia,
Mtu bora kujijua, na hadhara kuijua,
Wapo wa kushangilia, kwa malipo kugaiwa,
Aali wastahili, tumeangusha wananchi !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment