Sunday, November 6, 2011

Udaktari si hoja

Kuna digrii za bandia, nyingine za kupewa,
Dukani huko India, si vigumu kununua,
Kisomo lebo haijawa,bali uwezo nao kuwa,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Wengi tunaowajua, udakta wajivunia,
Ndani ukiangalia, hawana wanalojua,
Kitu wangelitambua, masikini tusingekuwa,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Ni sponchi zilojaa, maji huya kumwaia,
Pulizo zilopepewa, upepo ndani kujaa,
Abyadhi kifungua, akili zimetopea,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Udokta bwana kujua, kila unachoangalia,
Na unayojisemea, kuhakiki unajua,
Na kila unachosikia, tathmini kukifanzia,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Hesabu huzitambua, japo hutozielewa,
Kujumlisha sanaa, na kuzidisha hatua,
Ni mtu wa kutambua, mfuko sio gunia,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Si wa kuwaitikia, wachimvi wanaolia,
Wanasiasa kugwaya, kufanza wanayoamua,
Japo ujinga wajua, bado unawatumikia,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Sio kashfa nazua, watu budi kujijua,
Nafasi kutochukua, mahala pasipowafaa,
Na ushaur kujitia, hali huna unalojua,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Huruma ninawaonea, dokta jina kupewa,
Wengi wachangamkia, hata tiba asilia,
Marais waingia, ni nyingi wajizolea,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Mawaziri nao pia, sasa wanajipatia,
Wengine wazinunua, nafasi kujiongezea,
Mbumbumbu walokuwa, sasa ni maprofesaa,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Ila anzali ajua, hujui hujayajua,
Na kilemba si kofia, na wigi sio upaa,
Kibla wanaojua, uongo hawatazua,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

No comments: