Sunday, November 6, 2011

Mikoa tusipoamka

Wajinga watatawala, mikoa tusipoamka,
Naitoa halahala, uchaguzi tunataka,
Ila pasiwe na hila, kiongozi kumuweka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Ukiritimba watula, vigumu kuneemeka,
Uchama sasa ni hila, mikoa inavunika,
Na wajuu watawala, kile kisichostahika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Shamba la bibi walola, viongozi wastahika,
Kila mmoja apula, kile anachokitaka,
Si mashamba si mihela, wazidi kutakasika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Usimwamshe alolala, hilo wanalitamka,
Hawana kwako jamala, ila wao kulimbika,
Na hili kila pahala, hija sasa yafanzika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Madaraka kijumla, lazima kujayashika,
Mikoa kujitawala, kiuchumi kwa hakika,
Rasilimali ni ghala, ziache kuja ibika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Na huu si ukabila, kiongozi twamtaka,
Mkoa mwenye jamala, waziri mkuu kumweka,
Na mawaziri salala, wizarazo kuzishika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Na hili sio suala, wakubwa rai kutaka,
Ni ukoloni wa msala, kuacha hawatayataka,
Wazidi kuwa madhila wadhani wanajengeka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Watu acheni kulala, mikoa kutawalika,
Ubwege nao ufala, bado hamjauchoka,
Mikoa sio jalala, wabovu kujawaweka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Tusiendelee kulala, mikoa ije jengeka,
Ujerumani kulola, haya yanavyofanyika,
Ni raha yangu Makilla, mikoa kuongozeka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.

Kuna digrii za bandia, nyingine za kupewa,
Dukani huko India, si vigumu kununua,
Kisomo lebo haijawa,bali uwezo nao kuwa,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Wengi tunaowajua, udakta wajivunia,
Ndani ukiangalia, hawana wanalojua,
Kitu wangelitambua, masikini tusingekuwa,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Ni sponchi zilojaa, maji huya kumwaia,
Pulizo zilopepewa, upepo ndani kujaa,
Abyadhi kifungua, akili zimetopea,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Udokta bwana kujua, kila unachoangalia,
Na unayojisemea, kuhakiki unajua,
Na kila unachosikia, tathmini kukifanzia,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Hesabu huzitambua, japo hutozielewa,
Kujumlisha sanaa, na kuzidisha hatua,
Ni mtu wa kutambua, mfuko sio gunia,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Si wa kuwaitikia, wachimvi wanaolia,
Wanasiasa kugwaya, kufanza wanayoamua,
Japo ujinga wajua, bado unawatumikia,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Sio kashfa nazua, watu budi kujijua,
Nafasi kutochukua, mahala pasipowafaa,
Na ushaur kujitia, hali huna unalojua,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Huruma ninawaonea, dokta jina kupewa,
Wengi wachangamkia, hata tiba asilia,
Marais waingia, ni nyingi wajizolea,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Mawaziri nao pia, sasa wanajipatia,
Wengine wazinunua, nafasi kujiongezea,
Mbumbumbu walokuwa, sasa ni maprofesaa,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

Ila anzali ajua, hujui hujayajua,
Na kilemba si kofia, na wigi sio upaa,
Kibla wanaojua, uongo hawatazua,
Udaktari si hoja, hoja umesoma wapi?

No comments: