Wazee mnatumiwa, kama fala mmekua,
Amkeni twawambia, asubuhi inshakua,
Yenu kusimamia, na sio kusimamiwa,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !
Wangapi wadhulumiwa, na yote tunayajua,
Serikali imekaa, pembeni yaangalia,
Vipi mwachaguliwa, harabu kuitikia?
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !
Wazee mmejaliwa, busara zimewajaa,
Historia mwajua, na nchi ilikotokea,
Na tunakoelekea, mwaweza mkakosoa,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !
Na tunakoelekea, mwaweza mkakosoa,
Wakubwa kuwaambia, njia mmeshakosea,
Safari mkiendelea, lazima mtapotea,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !
Mkikubali kutumiwa, ni nani kuwaambia?
Wao watakujadhania, eti njia wanaijua,
Wakafosi kupotea, jahazi mrama likawa,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !
Wazee nawatambua, hekima mmeshapewa,
Mengi mmeshagundua, na wapi tunakosea,
Kussema mkijaliwa, wengi watayasikia,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !
Mkianza Jumuiya, haya kuzungumzia,
Pia itawatetea, na kilio kikasikiwa,
Adha zikawapungua, mkapata kupumua,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !
Wednesday, November 30, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment