Wajinga watatawala, mikoa tusipoamka,
Naitoa halahala, uchaguzi tunataka,
Ila pasiwe na hila, kiongozi kumuweka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Ukiritimba watula, vigumu kuneemeka,
Uchama sasa ni hila, mikoa inavunika,
Na wajuu watawala, kile kisichostahika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Shamba la bibi walola, viongozi wastahika,
Kila mmoja apula, kile anachokitaka,
Si mashamba si mihela, wazidi kutakasika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Usimwamshe alolala, hilo wanalitamka,
Hawana kwako jamala, ila wao kulimbika,
Na hili kila pahala, hija sasa yafanzika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Madaraka kijumla, lazima kujayashika,
Mikoa kujitawala, kiuchumi kwa hakika,
Rasilimali ni ghala, ziache kuja ibika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Na huu si ukabila, kiongozi twamtaka,
Mkoa mwenye jamala, waziri mkuu kumweka,
Na mawaziri salala, wizarazo kuzishika,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Na hili sio suala, wakubwa rai kutaka,
Ni ukoloni wa msala, kuacha hawatayataka,
Wazidi kuwa madhila wadhani wanajengeka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Watu acheni kulala, mikoa kutawalika,
Ubwege nao ufala, bado hamjauchoka,
Mikoa sio jalala, wabovu kujawaweka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Tusiendelee kulala, mikoa ije jengeka,
Ujerumani kulola, haya yanavyofanyika,
Ni raha yangu Makilla, mikoa kuongozeka,
Mikoa tusipoamka, kuzidi kudidimia.
Saturday, November 5, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment