Sunday, September 19, 2010

Wewe kwangu kama mfu

Wapo wanaopumua, lakini sawa na mfu,
Wasiokusaidia, bali huwa wanakifu,
Hata tajiri wakiwa, mali yao ni nyamafu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Vibaya kukumbukia, mafao safu kwa safu,
Niliokwisha watendea, watwana na marufu,
Nikashukuru dunia, kunikidhi ukunjufu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Nikashukuru dunia, kunikishi ukunjufu,
Nimesahau mamia, ila wangu udhaifu,
Kwalo ninashangilia, na kumtukuza Afu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Elimu nilowapatia, wakapata utukufu,
Kazi nilowaombea, wakazihodhi tarafu,
Mchango nilochangia, wakapata masurufu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Ni Vero ninayemjua, nyuma aliyerudufu,
Akazileta hidaya, kwangu na mai waifu,
Machozi tuliyaachia, kuipata hii sharafu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Wengi tumesaidia, ila huyu bashrafu,
Ni kazi kumpatia, na kula naye kandafu,
Moyoni katuchukua, masafa yenye urefu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Ni wengi waliokuwa, wafupi pia warefu,
Chetu tuliwamegea, pasipo ya israfu,
Nafasi tukawaachia, masafu kwa masafu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Leo waturingishia, kwa vito na zao sufu,
Kila wakiangalia, wajiona watukufu,
Na sisi watuzomea, masikini wa siafu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Tumeijua dunia, na nyoyo zake hafifu,
Tunashika yetu njia, hatuyataki madufu,
Msije tuparamia, tutawaona uchafu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

Ukimya tumechagua, sisi si watu wa rafu,
Wetu usipowaangalia, kwetu wewe kama mfu,
Kuna tunayemtegemea, naye ni wetu Latifu,
Wewe kwangu kama mfu, haupo kwenye dunia.

No comments: