Wednesday, September 22, 2010

Baradhuli awe nje

Awe nje baradhuli, akiwa ndani nazaa,
Hudhoofu yako hali, kwa mashaka na balaa,
Kasema Akilimali, nami ninalitambua,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani ni balaa.

Si mme si mwanamali, ni watu wa kuduwaa,
Ukweli hawakabili, uongo wanauvaa,
Hodari kwa ubahili, na wagumu wa kutoa,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani ni balaa.

Si watu wa afadhali, nafuu hawajaijua,
Hawana mustakabali, mambo yao ya kuzua,
Hesabu sioi kamili, ni watu wa kupungua,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani ni balaa.

Akiwa ndani ajali, hutoacha kuzijua,
Na yake kubwa dalili, uwazi kuukataa,
Mbishi kama kandili, iliyo kwenye mvua,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani ni balaa.

Amana hastahili, si mtu wa kuaminiwa,
Hulka yake dhalili, si mtu wa kusikia,
Hujiona kuwa ghali, kumbe bure hatofaa,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani ni balaa.

Shairi hili nakili, lafaa kuwaimbia,
Ni mjinga baradhuli, si mtu wa kufikiria,
Aweza kuwa na mali, na ovyo ikapotea,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani ni balaa.

Aweza kuwa jamili, mzuri wa kuzuzua,
Kimkaribia kimwili, utataka kukimbia,
Ni haramu si halali, hali yake alokuwa,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani ni balaa.

Kaditama sihimili, mbele siwezi endelea,
Nimemvua baradhuli, joho analotumia,
Muulizeni maswali, kama mtamuelewa,
Baradhuli awe nje, akiwa ndani balaa.

No comments: