Sunday, September 26, 2010

KWETU KUPENDWE KWANZA

NCHI kuiendeleza, ni watu kuwanyanyua,
Kwanza ukawatanguliza, vingine vikafuatia,
Huwezi haya kufanza, mzawa nyuma akiwa,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Kiongozi mjikweza, yeye akatangulia,
Hata angelihimiza,hawezi kufanikiwa,
Nchi ataipoteza,jangwani ikabakia,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Wageni ukiwakuza, wao wakatangulia,
Nchi utaidumaza,na mwishowe kudidimia,
Hao si watu wa kukwazwa,mwishowe hujiondokea,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Uzawa wanaobeza, dunia hawajaijua,
Huwezi kujiegemeza,kwa huyu mpita njia,
Nendeni mkichunguza,popote kwenye dunia,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Watu anayepuuza, kuwadharau wazawa,
Ni kiongozi wa giza,kapewa bahati mbaya,
Ni chakula cha mafunza, jina lake litaliwa,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Mzungu si mwanawenza, bure kumtumainia,
Na wengine wachuuza, Uchina pia India,
Mzawa akiwa kwanza, huna kinachopotea,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Mteza kwao hutunzwa, wahenga watwambia,
Hili kaa waliwaza, akilini kuingia,
Nchi bora hufanyiza, watu wakaifurahia,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Mkaa na mjibanza, hawajatufanania,
Na chungwa haliwi chenza,na utamu sio sawa,
Na asiyemjua pweza,kitoweo hukataa,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Nyenzo tunayoiwaza, si mtu kumchukua,
Ni akili kufyonza,wajualo tukajua,
Ganda ukishamenyeza,mbali utalitupilia,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Ustawi utaanza, wetu tukiwatambua,
Wakawa wanaoongoza, na wageni waajiriwa,
Hawawezi kuongoza, wasiokuwa wazawa,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Kama nchi kuongoza, lazima awe raia,
Ajabu tunaifanza, uchumi nje kugawa,
Kama tumepatilizwa,hatujui cha kutoa,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

Mabingwa wanajiuza, kazi wanaozijua,
Hata wa Uingereza, twaweza kuwachukua,
Urussi huwezi saza,pamwe nako Romania,
Wakwetu wapendwe kwanza, ndiyo mbegu ya ustawi.

No comments: