Kuna kitu wanambia, nashindwa soma ishara,
Sauti hujaitoa, ninakuona kwa sura,
Kila nikikuangalia, ninahisi taathira,
Mbona sijakuelewa, siwezi soma ishara !
Mboni nimeyafungua, ninaiona taswira,
Ila bado kulijua, mwenzi linalokukera,
Macho yananambia, masikio yadorora,
Mbona sijakuelewa, siwezi soma ishara !
Ningekuwa natambua, anga ningeisakura,
Ulilo nalo kulijua, usiipate hasara,
Namii ningekusaidia, tena bila ya papara,
Mbona sijakuelewa, siwezi soma ishara !
Sauti ingeitoa, ningelitafuta dira,
Alama ungezitoa, maana ningeichora,
Jicho lingelibonyea, nisingefanya papara,
Mbona sijakuelewa, siwezi soma ishara !
Ishara yako ya kimya, naona kama ibura,
Na nikahi waivaa, sijaona yako sura,
Laiti ungeliivua, nje ya hii hadhira....
Mbona sijakuelewa, siwezi soma ishara !
Kucheza ninazurura, mgumu huu mpira,
Wapi kuupelekeza, kulipata goli bora?
Nimebaki nazubaa, wengine watanipora,
Mbona sijakuelewa, siwezi soma ishara !
Sunday, September 26, 2010
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment