Wednesday, September 15, 2010

Mkuu wa mkoa vipi ?

1.
Kiongozi kazi yake, kutatua matatizo,
Ukijenga uezeke, tena utumie nguzo,
Madaraka usishike, kama fikra hamnazo,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
2.
Au huoni tatizo, wakati yakuzunguka,
Ofisi ni kipoozo, toka nje kugutuka,
Teremka ngazi hizo, hadi chini ukafika,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
3.
Wewe Waziri mkuu, mkoa yako milki,
Acha tu ya kunukuu, ingia katika mikiki,
Silaha yako mguu, kwalo haudanganyiki,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
4.
Wewe mkubwa gavana, milioni wako chini,
Hili na lile hawana, wakungoja mitaani,
Hatua iwe amana, njoo nawe mstarini,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
5.
Mkuu onyesha njia, watu wataifuata,
Ikiwa wanapotea, basi wewe ni matata,
Panga kisha kupangua, hatuutaki ukata,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
6.
Jamii iwe na nyumba, wameyachoka manyatta,
Pambanueni vihamba,watu wapate karata,
Siasa zile za kuimba,hazina wa kufuata,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
7.
Barabara kazi yako, zijengwe ima fa ima,
Juu wako nyuma yako, wewe sema waja hima,
Wala msikae kitako, hadi iishe zahama,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
8.
Miradi anzisheni, kama vile kampuni,
Watu wajumuisheni, hisa ziwe maishani,
Na pasiwe na utani, lazima mle yamini,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
9.
Miundombinu anzeni, juu nao wamalize,
Kusubiriana acheni, wenyewe sasa mjikaze,
China kajifunzeni, wanavyofanya seuze,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
10.
Juzi wamejenga treni, iendayo sana kasi,
Wameiga kwa Wajapani, ufundi pia asasi,
Kama vile ni utani, safari zao fususi,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
11.
Nendeni India muone, watengeza kila kitu,
Ni mikoa ya wajane, walakini watukutu,
Wanakua mara nane, sisi kwao hatufutu,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
12.
Paeni nako Brazili, mashine wakokotoa,
Kila kitu ni sahili, wazalisha kwa mamia,
Hawanao ujahili, milango wamefungua,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?

No comments: