Saturday, September 18, 2010

Majivuno Kusadikika

Kila mwabudu Wazungu, kujiamini kahama,
Kila mtegemea ndugu, kusimama keshakwama,
Asiyekitunza chungu, hifadhi hana daima,
'Weupe wa nywele zangu, hauonyeshi hekima:
sikiza kauli yangu, maamuzi na azma!'

Asiyemwogopa Mungu, shetani anamtuma,
Asojali watu wangu, hana ya kwangu heshima,
Achanganyaye mafungu, ni mwizi wa mali ya umma,
'Weupe wa nywele zangu, hauonyeshi hekima:
sikiza kauli yangu, maamuzi na azma!'

Atawalae kwa rungu, kuua kwake lazima,
Asotishika na mbingu,ardhi humsakama,
Hofu ikitiwa pingu,uoga hurudi nyuma,
'Weupe wa nywele zangu, hauonyeshi hekima:
sikiza kauli yangu, maamuzi na azma!'

Dunia ya wanguwangu,huipoteza hekima,
Nje kukiwa ukungu, huoni kwa kutazama,
Na utamu wake dengu, si utamu wa mtama,
'Weupe wa nywele zangu, hauonyeshi hekima:
sikiza kauli yangu, maamuzi na azma!'

Copyright © Sammy Makilla-2010

No comments: