Wednesday, September 15, 2010

Uponyeshe moyo huu

Kurudiana wataka, ombi sintolikataa,
Nafsi haina wahaka, ila moyo waugua,
Ni lazima kutibika, kabla sijauambia,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Kisa chake kuvunjika, wewe chote wakijua,
Ni pale ulipokiuka, za kwetu wenyewe sheria,
Na ukubwa kujivika, kujifanya unajua,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Kwa hasira kuropoka, na mambo kuuzulia,
Vibaya kukereheka, na kuchukia dunia,
Asubuhi kuamka, ukawa umekukataa,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Ukaapa na kuapika, hutoweza kurudia,
Utawa ukautaka,na misheni kuingia,
Na upweke kujivika,hadi mwisho wa dunia,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Ulikufa ukakuzika, na matanga kuanua,
Mara wazuka mzuka, huko ulikotokea,
Bado makubwa mashaka, hakika haujaijua,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Vipi nitaeleweka, moyo kuuangukia,
Nini kilichofanyika, hadi wewe kukuridhia ?
Mbona wanipa mashaka,ya balaa kulizua ?
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Wengi tumedanganyika, kwa hao viruka njia,
Na tukijakugutuka, hakifai kitumbua,
Mchanga kimeudaka, kula hakitokufaa,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Nilikupenda hakika, nawe hili walijua,
Nikakushika kikaka, ndugu kukuchukulia,
Uhaini kukuteka, hilo sikulidhania,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

Nierevushe Rabuka, hatua ya kuchukua,
Moyo wako umechoka, haupendi kuumia,
Upweke unautaka, kuachana na dunia,
Uponyeshe moyo huu uliokwisha kuuvunja !

No comments: