Sunday, September 26, 2010

Weupe ukiupenda

Binadamu kama nunda, kazi kustaarabika,
Mwenyewe anajiponda, hawezi kustahika,
Ni mwepesi kwa kuvunda, pasiwwe anayemtaka,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

Weupe ukijisunda, weusi hautaushika,
Ukikutoka udenda,ving'aravyo kupendeka,
Weusi utakushinda,katu hautathaminika,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

Na mkubwa kwa kutenda, viongozi Afrika,
Uti umeshawapinda,vyao kutokuthaminika,
Zimwi wanayemuunda,ndiye huja kuwazika,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

Akili hazijasarenda,mtunzi bado nakoka,
Si wote kuheshimika,wengine hao wavunda,
Mzima havai sanda, ila aliyelaanika,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

Weupe mnaopenda,ndo kamba ina kiraka,
Na pale ulipopinda,ndipo utapokatika,
Sio kazi yake randa,kabati kuunganika,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

Umesheheni vidonda,weupe hutofumbatika,
Haujakivika chanda,pete isochukulika,
Na hawa sio ya kutanda,pasipo kuthaminka,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

Hilo tisa bado kenda, okota cha kupukutika,
Haushikiki mlenda,bila ya kubwabwajika,
Nchi bora hujaunda,pasipo ya Mwafrika,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

Chetu lazima kupenda, na kwetu kukapendeka,
Kama hili hamkufundwa, taifa litaanguka,
Hakuna wa kutupenda, wenyewe tusipojitaka,
Weupe ukiupenda, weusi hudhalilika.

No comments: