Wednesday, September 15, 2010

Kilicho'za kimeoza

Kilicho'za kimeoza, hakiwezi acha nuka,
Kunukia miujiza,hata marashi 'kipaka,
Huzuii la kuoza,hili lataka kuzika,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Hata marashi puliza,harufu haitotoka,
Cha kuoza cha kuoza,tabia yke kunuka,
Chongo halwi kengeza,ndivyo ilivyo dunia,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Cha kuoza kimeoza,acha kuhangaika,
Japo alikuwa mwenza,hutoweza kumshika,
Kwa nisai na ajuza,desturi ni kuzika,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Kwangu kinachotatiza,hali ilivyobadilika,
Wangali hai waoza,kwa tabia na hulka,
Hali hii yawaponza,watu hai wananuka,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Uchu wa cheo waiza,macho wengi hupofuka,
Mwenyewe hujilemaza,kuvaa kustahika,
Siachi kujiuliza,vipi atasetirika ?
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Waungu wajitangaza, na hali wananuka,
Kaumu wanaibeza,eti wanatamanika,
Maiti sasa ni wenza,kitandani twashereheka,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Fisadi twapatiliza,huku tunajumuika,
Tena twazidi wakuza,daraja wanazovuka,
Likija ingia giza,sijui nani atatoka,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Wavivu tunawaoza,kwa vyeo kuwajibika,
Ajizi zinapoanza,jukwaani twalalamika,
Malezi yetu yakwaza,jamii kutajirika,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Vigumu nawaeleza,nchi kuweza jengeka,
Huku tunafuga funza,madaraka kuja shika,
Vidole kuviongoza,twende tunapopataka,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.


Kuzoza nilikizoza,si mtu wa kusikika,
Hodari waliojifanza,waona wameelimika,
nini utachowafunza,waweze tena kushika,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

Yangu sasa namaliza,cheo sitaki kushika,
Najificha na ajuza,shaibu nimetosheka,
Anijalie Muweza,hatima kurehemeka,
Hata upake marashi,kilicho'za kimeoza.

No comments: