Wednesday, September 15, 2010

Mnavyowapenda wenu

Laiti sisi wakata,tungelikuwa na chetu.
Tuwe wa kunatanata,zinawiri hali zetu,
Wenetu tungepakata,tuwalishe kila kitu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Malaika nakuita,mpendwa wetu mwenetu,
Njoo machozi kukufuta,hao tena si wenzetu,
Kipato chao chatweta,hatujaweza kufutu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Elimu tutajiburuta, uwe na watoto wa watu,
Zaidi tukikipata, hilo lisiwe deni kwetu,
Tungali tunatafuta, benki tena hatuna kitu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Wakubwa wameukata, jamaa sio wenzetu,
Azimio walifuta,ili tusipate kitu,
Ujamaa kuuchota,mazingaombwe kwetu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Zao turufu karata,geresha zote ni zetu,
Na sasa wanyatanyata,usultani jadi yetu,
Hatosana mwana mkata,ila utumwa ni wetu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Miaka itawasuta, ngoja nikwambie kitu,
Itajazusha utata, mvi zikaota kutu,
Migongo kuwakong'ota, akili zikawa butu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Kwa njaa mtajapeta,muukamate wenu utu,
Hapo hakuna kuteta,ila fukia sepetu,
Mguu tupu kuuwata,uje kuvaa viatu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Zama nilishakuita, uje ulimwengu wetu,
Miaka mingi kupita, ukawa kwenye msitu,
Sauti hukuipata, kwa dhiki za mtutu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Rwanda nilikwishapita, kuwasalimu Wahuru,
Watutsi wakaniponda, eti wale si wenzetu,
Kumbe kiyama waita,jinsi walivyothubutu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Kenya nilishawasuta, wakaniona si mtu,
Kuondoka kwa Kenyatta,kamwachia mtukutu,
Vilio anayeviita,maana si mtu wa watu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Kibaki alipogota, Mungiki akawa chatu,
Odinga naye kanyata, akiyakwepa matatu,
Kisumu hadi Mvita, ikatembea mitutu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

Ndoto hatujaiota, hapa kisiwani kwetu,
Amani tumeichota, hauvuji mtungi wetu,
Ila mizimu yaita, kila msiba na tatu,
Mnavyowapenda wenu, ndivyo tungependa wetu.

No comments: