Wednesday, September 15, 2010

Diwani fungua macho

1.
Waweza boresha kata, si kama ilivyokua,
Yaweza isha matata, kata ikajitanua,
Wawza maliza ukata, kampuni mkikwaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
2.
Diwani ni kama nta, umoja ukatokea,
Hamasisha wana kata, vikao wapate kaa,
Maamuzi kuyakata, mengi yenye manufaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
3.
Maendeleo ni vita, katika yetu dunia,
La sivyo mtapakata, umaskini sawia,
Neema hamtoipata, hadi mwisho wa dunia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
4.
Kata lazima kuota, ndoto zenye majaliwa,
Msikubali kusota, wengine wanakimbia,
Boresheni Mkukuta, muweze kuja kupaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
5.
Wenngine wanawasuta, na pia kuwanyanyapaa,
Neema hamjatafuta, vijiweni mnakaa,
Za mchana mnaota, ndoto zisizowafaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
6.
Fikra hamjapepeta, rai kuzichanganua,
Yapo mambo mia sita, chache mwaweza chagua,
Na hapo mkajikita, mazuri kukokotoa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
7.
Ubinafsi wawasuta, madalali wa mitaa,
Mwauza hata viota, wapi ndege watakaa?
Historia mtadata, itawachora vibaya,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
8.
Diwani acha kuteta, neema budi kuzua,
Na wala usije ota, utakuja kuizoa,
Haipati maji kata, bila mtungini kwingia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
9.
Usiwe wa kupitapita, majilisi hujakaa,
Wakazi nao kuteta, ndio njia ya kuanzia,
Mawazo mkayavuta, matatizo kugundua,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
10.
Ufumbuzi kutafuta, kero zilizoenea,
Diwani kavae ngata, mtungi kichwani tia,
Na kama kucheza kwata, gwardi kuparamia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
11.
Diwani usiwe mtata, mtu wa watu jua,
Madhambi yote kufuta, wewe yakutegemea,
Itakate yenu kata, ing'are kuliko sinia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
12.
Diwani rai tafuta, na elimu kimbilia,
Usijefanye dokata, la saba halijatimia,
Watakuona kiputa, nundu kuja kukulemea,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
13.
Natupa yangu karata, geresha halijanifaa,
Ukiona unatota, bafuni hujainigia,
Basi tambua mafuta, mwilini yamezidia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!

No comments: