Thursday, September 16, 2010

Mweupe Kisha Mweusi

1.
China na Malaysia, wameshaoneysha njia,
Himaya wamejijengea, wananchi kutangulia,
Viranja wakabakia,wa mwisho kuangaliwa,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
2.
Kwao wamemuondoa, mkoloni kakimbia,
Na wao hawakuchagua,kuwarithi walokuwa,
Taifa kutumikia,hilo ndilo waloamua,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
3.
Viongozi wetu baa,wajua wanalokimbia,
Ikulu wakiingia,kazi kujishaua,
Matanuzi kuyakwaa,hata yasiyowafaa,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
4.
Kitendawili kimekua,hamsini yatimia,
Wanavaa wanavua,wengine wanaingia,
Sala inatabiriwa,mwananchi ataumia,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
5.
Mweupe amwemwachia, mweusi tunayemjua,
Naye ashilindilia, shindilia dona kawa,
Viumbe wanatitia,ardhini wadidimia,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
6.
Mweusi kashikilia,ufalme katangazia,
Gabon wameamua,Misri wanafuatia,
Na pengine yatatokea, huko tulikozaliwa,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
7.
Hili haliwi ni baya, kama hai tungekuwa,
Kwa maana ya kuchanua, ustawi
tukakwea,Kilele kukifikia,cha waliokwishajaliwa,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
8.
Hawa wanalolijua, ni kula na kutumia,
Shilingi yadidimia, wao wanazidi jaa,
Nchi imeshafulia,twaambiwa yaendelea,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
9.
Bure ukiviachia, ni wapi utajazilia,
Benki ukizipakua, nani wa kukufidia,
Utapiamlo ukijaa, akili nani kujaliwa ?
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
10.
Akili zimeshavia, nani analo jipya,Mazezeta
tunshakuwa, kaburi latungojea,
Kasi imeshahasiwa, kipi kitakachozaliwa ?
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
11.
Hoi tumekwishakuwa,wapi nguvu kupatia,
Ari imeyoyomea,ni wapi pa kuanzia,
Ni budi upya kuzaliwa,mambo ndio kutangamaa,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
12.
Kama miji yasinzia,vijiji vimeishilia,
Usingizini vyarudia,Kuamka shida imekuwa,
Miujiza yangojewa,hali kujanusuriwa,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.
13.
Kizazi changu chalia, nchi tumeibambua,
Hakuna kilichobakia,gogo lote laishia,
Na wanaotufatia,lazima kushtakia,
Mkoloni rangi nyeupe, kamuachia Mweusi.

No comments: