Thursday, September 16, 2010

Dhahabu anachukua

1.
Sijui weusi baa, kama sio mgahawa,
Mjanja kumtania, hajui asiyejua,
Na nchi ikivamiwa, mamluki mwamjua,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
2.
Kunyonga aliyezoea, kuchinja anachelea,
Mwizi ukimchagua,jua atakuibia,
Mbwa ukimzoea,msikitini huingia,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
3.
Anayedharau wazawa,mwenyewe hajajijua,
Utuwe hununuliwa, mateka kisha akawa,
Kiongozi msifiwa, heri zezeta ya kuwa,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
4.
Vibaka tunawajua, walio kwenye mitaa,
Ila hatujawajua,ukubwa wanaouvaa,
Hazipishani tabia, kama hujui tambua,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
5.
Ujinga hautokufaa, mwizi kumng'amua,
Tende hukutupia,nawe ukanogewa,
Basi utamuachia,vya maana kuchukua,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
6.
Mwafrika kalaaniwa,au kachanganyikiwa,
Nduguze kuwakataa,kuona wasiofaa,
Wageni kushikilia,nasaba wasiokuwa,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
7.
Mikosi inashupaa, na maafa yatanua,
Nchi zinaangamia, waroho wachekelea,
Viongozi twachagua,wenyewe wanaojifaa,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
8.
Andiko hili radhia, lisome kizazi kipya,
Hao ndio watajua,ni nani wetu majuha,
Na kisha kuwazomea,kuzika hai wakiwa,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
9.
Waifute historia, yote waliochafua,
Walo wema kubakia, hadi siku ya kiyama,
Na Mola kushuhuhudia, Afu aliyetimia,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
10.
Hamsini yatimia, miaka ya kupotea,
Jangwani tulipagawa,na njia hatukuijua,
Leo Rabi twamlilia,nyota itaangazia,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
11.
Sisi katu hatujawa, ndio jaa la dunia,
Vya wengine kununua, nasi kutowauzia,
Akili zingepungua, uwizi tusingejua,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !
12.
Muda umekaribia, eon kuja kutimia,
Mwokozi mkimlilia,Mungu huwazawadia,
Wezi mking’ang’ania,naye atawaachia,
Dhahabu anachukua, anigawia mkaa !

No comments: