Friday, September 17, 2010

Akili kama vyoo

Ndio wetu viongozi, na hizi akili zao,
Wafurahia ushuzi, ukiwa kwa wengineo,
Wao yao matanuzi,kilo bora ndicho chao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Onyesha wao ushenzi,huja mbogo watu wao,
Mtu akitoa chozi, acheka hudai wao,
Mwananchi kwao masinzi, bora si yamfaayo,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Hutuiita wachochezi, nchi twataka pindua,
Kumbe wao wachokozi, kazi si wanaojua,
Ila kawapa Mwenyezi, uwezo sasa ni wao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Nchi imekosa wajenzi,tapeli watawalao,
Hawa ni wengi wa ajizi, heri sio waletao,
Umejaa ubazazi, ndio matunda yao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Tunataka mapinduzi, wa viongozi wajuao,
Wanaoheshimu kazi, za wananchi wenzao,
Wasotia pingamizi,habari wazitoao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Hatutaki mashauzi,majuha tulionao,
Wadhanio uongozi,ni kunyanyasa wenzao,
Tunataka chapakazi,popote wajitumao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Mahakama za wajuzi, sikia chetu kilio,
Waandishi na watunzi,kwa sasa tukitoao,
Tutashndwa fanya kazi, kwa vitishi na matao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Yafanyeni maamuzi, hawa si watufaao,
Nchi wapaka masinzi,kwa wote watujuao,
Twaonekana washenzi,na sheria si tujuao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Uongozi kubwa kazi, waulize wajuao,
Usidhani ni viyoyozi,maslahi na mafao,
Cheo ni usimamizi,uletao mafanikio,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Cheo ni uangalizi, wa wale uongozao,
Na ukubwa ni malezi, yaje bora matokeo,
Ukuu si maonezi, kwa cheo uwazidio,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

Utumwa hatuuwezi, miaka hii iwayo,
Wafalme si majazi, wala si tuwatakao,
Hatutaki viongozi, watu wanyanyasao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !

No comments: