Ndio wetu viongozi, na hizi akili zao,
Wafurahia ushuzi, ukiwa kwa wengineo,
Wao yao matanuzi,kilo bora ndicho chao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Onyesha wao ushenzi,huja mbogo watu wao,
Mtu akitoa chozi, acheka hudai wao,
Mwananchi kwao masinzi, bora si yamfaayo,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Hutuiita wachochezi, nchi twataka pindua,
Kumbe wao wachokozi, kazi si wanaojua,
Ila kawapa Mwenyezi, uwezo sasa ni wao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Nchi imekosa wajenzi,tapeli watawalao,
Hawa ni wengi wa ajizi, heri sio waletao,
Umejaa ubazazi, ndio matunda yao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Tunataka mapinduzi, wa viongozi wajuao,
Wanaoheshimu kazi, za wananchi wenzao,
Wasotia pingamizi,habari wazitoao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Hatutaki mashauzi,majuha tulionao,
Wadhanio uongozi,ni kunyanyasa wenzao,
Tunataka chapakazi,popote wajitumao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Mahakama za wajuzi, sikia chetu kilio,
Waandishi na watunzi,kwa sasa tukitoao,
Tutashndwa fanya kazi, kwa vitishi na matao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Yafanyeni maamuzi, hawa si watufaao,
Nchi wapaka masinzi,kwa wote watujuao,
Twaonekana washenzi,na sheria si tujuao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Uongozi kubwa kazi, waulize wajuao,
Usidhani ni viyoyozi,maslahi na mafao,
Cheo ni usimamizi,uletao mafanikio,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Cheo ni uangalizi, wa wale uongozao,
Na ukubwa ni malezi, yaje bora matokeo,
Ukuu si maonezi, kwa cheo uwazidio,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Utumwa hatuuwezi, miaka hii iwayo,
Wafalme si majazi, wala si tuwatakao,
Hatutaki viongozi, watu wanyanyasao,
Ubovu wa vyetu vyoo, sawa na zetu akili !
Friday, September 17, 2010
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment