Thursday, September 16, 2010

Tumbo likiuma….

1.
Muone akitembea, utadhani ni maswezi,
Guu ashindilia, utafikiri mjenzi,
Kiuno kashupalia, mithili yake mkwezi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.
2.
Mja si yako dunia,tabia chako kitanzi,
Nini unachoringia,wengine hawakimalizi ?
Wajitakia ukiwa, siku yenye fumanizi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.
3.
Leo unavyotembea, iweje kesho huwezi,
Tumbo likivimbiwa,mbona itakuwa kazi,
Hubaki unalialia,na vishindo vya ushuzi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.
4.
Tembea bila umbeya,kama mtu wa zoezi,
Nenda waihurumia,dunia yake Mwenyezi,
Na wale wanaojua,ni amri ya Azizi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.
5.
Nenda unafikiria, na Manani kumuenzi,
Zipige zako hatua,dunia hauimalizi,
Kwa staha kutembea,na kusifu hii enzi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.
6.
Wanangu nawausia,dunia siyo ya machizi,
Elimu kuzisomea,mema yalo matembezi,
Mwenyezi nikumjua,njia hugeuka majazi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.
7.
Kuvimba haijakuwa,jambo lililo na radhi,
Ni bure kujitanua,bahari hauiwezi,
Yanini kujisifia,msifu wako Muizzi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.
8.
Watazame walokuwa,wakitamba na mabenzi,
Waliovimbisha vifua,walifunzwa hawafunzi,
Kimya wameshatulia,wameiafiki dozi,
Mbwembwe kwa kutembea, tumbo likiuma huwezi.

No comments: