Keshashiba sana paka, kuwala panya hataki,
Na nyama kafaidika, vya kuwinda havitaki,
Sharubu zimekunjika, kuruka tena haruki,
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Kakaa hana mashaka, na wala hapapatiki,
Mwenzetu kesharidhika, visivyopikwa hataki,
Msafi anajiweka, kujilambalamba hachoki,
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Paka amekwishafika, masikani habanduki,
Sasa keshazoeleka, ndani ya nyumba hatoki,
Wengine wanamtaka, kitandani hudiriki,
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Hajali anayemweka, anachojali riziki,
Hawezi akatoroka, kwani ametamalaki,
Wenyeji wanamtaka, kwanini awadhihaki?
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Paka ametajirika, ikulu ni mstahiki,
Ukubwa kajipachika, wadogo tena hataki,
Milki ameishika, uongozi ashiriki,
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Sio pusi huyu paka, walal jina nyau hataki,
Kaacha kuhangaika, inamfuata riziki,
Kazisusa patashika, kasri keshaiteka,
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Hajui yanayozuka, mapanya wazua baa,
Wazaliana hakika, ndani kote wameshajaa,
Ni nani wa kuwashika, na paka amekataa?
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Unaweza neemeka, kwa nyota yake twariki,
Kumbe ndio waanguka,u chini kitahamaki,
Yasiyemfika paka, huko alikokwishajaa,
Paka ameshiba mno, hataki kuwala panya !
Wednesday, September 22, 2010
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment